Saturday 5 November 2016

TUPA KULE: UCHUNGU WA KUZAA KWA WANAWAKE

DUNIA  iliyokuwa inatambaa kwa sasa inakimbia tena inakwenda kasi kama upepo wa jangwani, na yale tuliokuwa tunayaita maajabu kwa sasa si maajabu tena
Maandiko ya Dini yanasema  mwanamke atazaa kwa uchungu lakini wanawake wa siku hizi wamekuwa hawataki kuzaa kwa uchungu na badala yake wanatafuta dawa na njia mbalimbali kuhakikisha kuwa wanajifungua kwa raha mustarehe. 

Wapo wanawake wengine ambao wanadiliki kuwaomba madaktari wawazalishe kwa kisu mara tu mtoto anapotimia ili mradi kukwepa maumivu ya uchungu ambayo mama hukumbana nayo wakati wa kujifungua. 

Wakati wanawake wakiamua kuzaa kwa njia ya upasuaji ili kukwepa maumivu ya mtoto kutoka tumboni, wanasayansi nao wamegundua njia mbadala ya kumfanya mwanamke asihisi uchungu wakati wa kujifungua. 

Wamegundua kuwa nyoka mwenye sumu kali zaidi duniani huenda akawa jibu la kupatikana kwa dawa ya kupunguza uchungu. 

Nyoka anayeitwa ‘Blue Coral’ ndiye mwenye sumu kali zaidi duniani na anapatikana zaidi Kusini Mashariki mwa Bara la Asia ambapo utafiti mpya uliochapishwa katika jarida la afya la Toxin umesema kuwa nyoka huyo huwalenga maadui wake ambao husababisha uchungu kwa binadamu. 

Wanasayansi wanaeleza kuwa huenda sumu ya nyoka huyu ikatumika katika kutengeneza dawa ya uchungu na baadhi ya wanyama ambao sumu yao imetumika kutengeneza dawa ni pamoja na konokono waishio baharini ama buibui wenye sumu kali. 

Kwa sasa wanasayansi wanataka nyoka huyu ahifadhiwe hasa hususan baada ya maeneo mengi anakopatikana kugeuzwa kuwa mashamba ya michikichi huku wanasayansi hao wakifanya utafiti wao kwenye nchi za China, Singapore na Marekani. 

Watafiti wanasema japo kwa mwanadamu nyoka huwa adui, lakini wakati huu huenda akawa suluhu la matatizo mengi ya kiafya.

No comments: