Saturday 19 November 2016

CHOZI LAKO



Naitafakari siku, ilivyoishia vema
Tena Kwa nyingi shauku, nilitamani kusema
Na hali yangu kapuku, akili ikazizima
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani

Anililiaye nani, kwa uchungu wa mapendo
Nalijihisi katuni, tena nisiye vishindo
Nitesekae jangwani, nisipate maji fundo
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani

Kutangatanga msafiri, nisietua mizigo
Ninazipanga safari, zilizo nyingi mitego
Sasa natafakari, ingawa mekupa zogo
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani
Neno gani nikwambie, huenda ukaelewa
Unisikilize mie, tayari nimechachawa
Ububu nijivikie, usije ona melewa
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani
Nalikutoa machozi, na wala sikukufuta
Yalidondoka kwe ngozi, hukutaka kupukuta
Nilijifanya ajizi, nisiyejua chakufata
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani
Asante kwa chozi lako, limeniweka furahani
Najua thamani yako, sitokutoa moyoni
Sikuliliwa mwenzako, wewe wa kwanza amini
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani
Ujuaye hali yangu, na bado ukathamini
Nakuapia kwa Mungu, sitaitema amini
Sitayasikia majungu, wakitema midomoni
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani
Sijui nawaza nini, kujibu yaso kichwani
Nashukuru ukibaini, niyasemayo betini
Ndiyo yaliyo moyoni, tena hayo ya sirini
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani
Huruma  pendo la kweli, hujifichama moyoni
Huna jicho la tapeli, kujisafi tu usoni
Huzuni yako ya kweli, naitazama machoni
Asante kwa chozi lako, nimeijua  thamani


By Fulgence Makayula

No comments: