Sunday 29 May 2016

KILIMO CHA MPUNGA CHAWAKOMBOA VIJANA



https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjLEcXbVm9KfsCNlonWWqzov4pnbGQyIJQ8e7jOryPw4AVDHPvwycnTSUOW2lSfHVaO978cWGOesEtWdOnWjSMJSwsi-CHHnw-4hNOjnN7R94x2biGMTUrT9Re0TKwanIRPzfzzppJZBgY/s1600/DSC00487.JPG
Mkulima wa Mpunga akifurahia sehemu ya kazi yake huko Mkoani Ruvuma hivi karibuni
Na, Fulgence Makayula

Kilimo ni uti mgongo wa taifa la Tanzania ambapo takribani asilimia 60 ya watanzania wote uishi kwa kutegemea kilimo ambacho kimekuwa mkombozi mkubwa wa maisha yao.
Huku kukiwa na mgawanyiko mkubwa wa maeneo na mazao ya kilimo maeneo ya kanda ya kaziskazini kilimo cha mazao ya biashara kama vile kahawa kililimwa kwa wingi pamoja na mazao ya chakula kama vile mahindi, matunda na viungo kama nyanya, vitunguu, tangawizi na vinginevyo vingi vikilimwa huko.
Kwa kanda ya ziwa kilimo cha mazao ya biashara ikiwemo pamba na kahawa kwa mkoa wa Kagera, mazao ya chakula kama mtama, mahindi, viazi vitamu, uwele na mihogo ndiyo mazao makuu ya chakula yalimwayo kwenye mikoa hiyo ya kanda ya ziwa.
Lakini kwa kanda nyingine pia mahindi hulimwa kwa wingi, Alzeti kwa mikoa ya Singida na Manyara kwa kiasi fulani, Morogoro pia hulimwa mpunga kwa wingi kama ilivyo kwa mikoa ya kanda ya Juu kusini hususani mkoa wa Mbeya.
Kwa takwimu zilizotolewa kutokana na Sensa ya Watu na Makazi iliyofanyika mwaka 2012, inaonyesha kuwa zaidi ya asilimia 65 ya watanzania wote hutegemea kilimo ili kuendesha maisha yao bila kujali ni kilimo cha aina gani. Huku wazalishaji wakubwa wakiwa ni wakina mama ambao ushughulika na shughuli za kilimo ili kukomboa familia na bara zima la njaa na umaskini.
Lakini cha kushangaza hapa vijana ambao wapo zaidi ya asilimia 54 ya watanzania wote huku wakiwa na nguvu za kutosha kutumika na kujenga nchi hii kwa kutumia rasilimali zilizopo nchini hususani Ardhi. Wengi wao wamekuwa wakikimbilia mijini na kuwaacha wazazi wao wakiwatafutia mahitaji na kuwategemea kwa asilimia kubwa.
Kundi kubwa la wanaoenda mijini hujiusisha na shughuli za kiuharifu ikiwemo uvutaji wa bangi, ukabaji na uporaji na majanga mengi ikiwemo lile la kujiuza kwa baadhi ya dada na wakaka ambao ujulikana kwa majina maarufu ya machangudoa na makakapoa.
jambo hili limekuwa tofauti kwa kijana Kelvin Chombo ambaye ni mwanafunzi wa chuo kikuu kishiriki cha Elimu Dar Es Salaam ( DUCE), ambaye ameitumia vizuri fursa ya kilimo  kwa kuanza kulima kilimo cha mpunga. Ambacho yeye mwenyewe anaamini ndicho kilimo kitakachomkomboa na kumfanya awe na maisha mazuri ya mbeleni.
 Na si kubaki kuishi maisha tegemezi kama vijana wengine waishivyo kwa kubweteka na kusahau kujishughulisha na shughuli za kilimo kwa kuogopa kuchekwa au kuonwa wa zamani maana wapo baadhi wana dhana potofu kuwa mtu aliyesoma si sahihi kujiusisha na masuala ya kilimo.
Kelvin alianza kujishughulisha na kilimo cha mpunga tangu mwaka 2009, akiwa kidato cha pili huko Mkoani Morogoro,ambapo tangu kipindi hicho amekuwa akipata mafanikio makubwa ambayo yanamwezesha kuishi maisha ambayo yeye anaamini kwa kiasi kikubwa ni ya kujitegemea kwa takribani Asilimia 70.
‘‘Nilianza kulima mpunga tangu nikiwa kidato cha pili mwaka 2009, ambapo nilikuwa nalima ekari moja ili kujipatia mahitaji yangu ya shule na chakula cha pale nyumbani. Lakini hii ilichangiwa na  wazazi wangu kuwa wakulima hivyo tulishirikiana kulima mazao mbalimbali kama choroko, migomba, mahindi na mazao mengine ya chakula yakiwemo maharage. Lakini zao kubwa lilikuwa mpunga ambalo kwa kiasi kikubwa tulilitegemea na huchangia kupata mahitaji mengi ya shule ikiwemo ada na baadhi ya mahitaji ya shule hii baada ya kuuza mpunga msimu wa mavuno”
Kelvin anasema, “ hauwezi kuamini nipo hapa chuo lakini bado najihusisha na kilimo ambako kwa sasa nina ekari tano, ninazomiliki mwenyewe, huwa nazilima kipindi cha likizo. Na ninapokuwa chuo wazazi wangu hunisaidia uangalizi wa mashamba yangu, kwa mfano likizo hii iliyoisha majuzi ya muhula wa kwanza. Ambapo tulifunga chuo kwa muda wa wiki tatu nilienda kufanya palizi ya shamba langu na kuweka mbolea pamoja na dawa kuuwa magugu”
“Kiukweli nimefanikiwa sana kupitia kilimo na ndicho kinaniwezesha kujilipia ada yangu hapa chuoni, maana Serikali inanipatia fedha za kujikimu,  chakula na malazi ila ada najilipia mwenyewe, pia nasaidia familia yangu pamoja na wadogo zangu na huwa siwasumbui wazazi wangu suala la ada wala matumizi labda niwe naumwa au kuishiwa kabisa ambap[o huwa ni kwa nadra sana kutokea”
Akiwa ni mzaliwa na mkazi wa Mtimbira mkoani Morogoro, amekuwa taa na mwangaza kwa  vijana wengine ambao huenda wameshindwa kuchukua hatua za kujishughulisha na kilimo. Hivyo wanaweza kuona  fursa hii ambayo itawakwamua kimaisha. 
Mbali na hayo Kelvin anaendelea kuwaasa vijana wenzake kuwa , “kilimo ni kizuri mno maana ni ajira isiyo tumia gharama kubwa na mtu unaweza  usiwe na mtaji wowote zaidi ya mbegu, mtaji ni nguvu zako. Hii ni shughuli ambayo inamuingizia mtu kipato pasipo kuwa na gharama kubwa ya kianzio.
 Maana vijana wengi wanashindwa kujitoa wakidai hawana mtaji, lakini kwenye kilimo hakuna kusema kwamba unahitaji mtaji mkubwa kiasi gani, kama mwenyewe pia unajishughulisha basi utajikwamua katika hali ya utegemezi na hatimaye msimu ukifika unapata kianzio chako.  Sasa kama unataka kutoka kwa mtaji basi hapo sasa kilimo kinakupatia mtaji.” 
Na kuongeza kwa shairi moja maarufu ambalo linaitwa kama unataka mali utaipata shambani, maana hakuna mbadala wa shamba maana waswahili usema mtaji wa maskini ni nguvu zake mwenyewe.
Na anatumia mwanya huu kuwasihi vijana wenzake kuepukana na mawazo mgando, na badala yake waone kilimo kama ni fursa pekee ambayo pia inaweza kuwatafutia mtaji wa kujiajiri wenyewe.
John Nyaluchi, ni rafiki mkubwa wa  Kelvin ambaye wanasoma naye chuoni hapo yeye anasema “ nimemfahamu Kelvin kwa muda mrefu sasa, na amekuwa fundisho kubwa kwenye maisha yangu , jinsi anavyojishughulisha na shughuli za kilimo. Kwani nilipata fursa ya kwenda Morogoro kuona kama anachoniambia ni kweli, kwa kweli amekuwa fundisho kubwa si kwangu tu hata kwa vijana wengine hapa chuoni na nje pia.
Mzee Chombo ni baba mzazi wa Kelvin anasema “ nina muamini sana kijana wangu kwa kuwa tangu amejikita kwenye kilimo cha mpunga ametusaidia sana hapa nyumbani, hata wadogo zake maana muda mwingine nikikosa kabisa fedha ya kuwapeleka wadogo zake shule, nampigia simu anasema tuuze mpunga wake, na tunafanya hivyo” 
Hivyo basi vijana wa kitanzania ni vyema kuona fursa zilizo kwenye maeneo yao kwa kutumia rasirimali zilizopo nchini ikiwemo ardhi ambayo imejaa rotuba kwa kilimo cha mazao mbalimbali yakiwemo ya chakula, mbogamboga, matunda pamoja na mazao ya biashara ambayo yatainua kipato cha mmoja mmoja.
Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika na watu wake pia wakiwemo vijana wenye nguvu za kufanya kazi za uzalishaji mali. Ili kupunguza vitendo vya ubakaji, uporaji, uvutaji madawa ya kulevya, na kukaa vijiweni pasipo kujishughulisha.






No comments: